Watumishi wilayani Mafia wametakiwa kuzingatia maadili ya kazi katika utekelezaji wa majukumu yao ili waweze kuhudumia wananchi kwa uaminifu mkubwa.
Wito huo umetolewa Mei 24, 2025 na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mafia Ndugu Mussa Kitungi wakati wa sherehe ya wauguzi iliyofanyika katika Hoteli ya Base Camp, Utende ambapo sherehe hiyo ilienda sambamba na kukaribisha watumishi wapya wa Idara ya Afya.
Ndugu Kitungi ameeleza kuwa suala la ukosefu wa maadili kwa watumishi na jamii kwa ujumla ni adui mwingine kama ilivyo Ujinga, maradhi na umaskini.
" Sote tunafahamu maadui wakubwa watatu ambao ni Ujinga, Maradhi, na Umaskini, ila siku hizi ukosefu wa maadili nao ni tatizo kwa taifa letu" alieleza.
Aidha, ametilia mkazo suala la kutoa mafunzo kwa watumishi kwa kuwajengea uwezo pindi wanapoajiriwa ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa uwajibikaji, ubunifu pamoja na kuzingatia sheria, taratibu na miongozo iliyopo katika Utumishi wa Umma.
Ndugu Kitungi ameishukuru Serikali chini ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuboresha sekta ya afya pamoja na sekta nyingine kwa kuajiri watumishi ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Jumla ya waajiriwa wapya 90 wamepokelewa wilayani Mafia ili kupunguza uhaba wa watumishi wa sekta hiyo, hatua ambayo Serikali inaendelea kuchukua ili kuboresha sekta ya afya kisiwani Mafia na Taifa kwa ujumla.
Halmashauri ya Wilaya ya Mafia kupitia Idara ya Afya husherehekea siku ya wauguzi kila mwaka kwa kumuenzi Muuguzi Muingereza, Florence Nightingale ambaye alisifika kwa utendaji kazi wake katika karne ya 19.
Kilindoni-Bomani Street
Anuani ya posta: 85
Simu: 0232010199
Simu ya mkononi:
Baruapepe: ded.mafia@pwani.go.tz / ded@mafiadc.go.tz
Copyright ©2017 Mafia District Council . All rights reserved.